Mapigano yanaendela mashariki Congo DR

Unknown | Tuesday, November 20, 2012 | 0 comments

Mapigano mengine yamezuka  karibu na mji wa Goma huko Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo-DRC, baada ya serikali ya DRC kupuuza madai ya mazungumzo ya amani kutoka  kundi la waasi wa M23.
Mwandishi  wa habari wa Sauti ya Amerika-VOA anasema kulikuwa na ufyatuaji risasi mkali  Jumatatu  kiasi cha kilomita tatu kutoka  mji wa  Goma na karibu na uwanja wa ndege. Msemaji wa kundi la M23,Vianney Kazarama aliiambia VOA kwamba kundi la waasi linadhibiti sehemu ya kaskazini-mashariki mwa Goma.
Pia kuna ripoti za ufyatuaji risasi kwenye mpaka wa DRC na Rwanda. DRC inaishutumu Rwanda kwa kuwasaidia  waasi wa M23 huku Rwanda ikiendelea  kukanusha shutuma hizo.
Wapiganaji wa M23 wamesonga mbele kilomita chache kuingia Goma katika muda wa siku chache zilizopita baada ya kuyarudisha nyuma majeshi ya serikali na walinda amani wa  Umoja wa Mataifa.  Wakati huo  huo, Idara ya  Watoto ya Umoja wa Mataifa-UNICEF inasema vita vikali vinavyoendelea huko Goma mashariki mwa DRC vimelazimisha maelfu ya watu ambao tayari wamepoteza makazi yao  kukimbia kwa mara nyingine.
UNICEF inasema ina wasiwasi  juu ya athari za kisaikolojia ambazo watoto wa Congo watakabiliwa nazo.  Nona Zicherman  mkuu wa UNICEF anayeshughulikia masuala ya  dharura   huko Kinshasa anasema wasiwasi wao mkuu ni hali ya wanawake na watoto ndani na karibu ya Goma, ambao wameathirika na mapigano na  pia  wasiwasi juu ya usalama wa wafanyakazi wao.
Anasema maelfu ya watu tayari wamekimbia maeneo ya watu waliopoteza makazi yao kilomita kadhaa kutoka Goma.Zichermann anasema UNICEF  inajua kuwa kulikuwa na idadi kubwa ya raia waliokwenda Goma kutafuta hifadhi na kwamba walikuwa wakiwasaidia katika  kambi ya Kanyaruchinya iliyopo nje ya Goma  ambayo ni makazi ya takriban watu elfu 60.
Anasema japo hawana idadi kamili wanajua kuwa idadi kubwa ya raia wa Kanyaruchinya na vijiji jirani pia wamekimbilia Goma na wamefika katika sehemu kadhaa na wanaishi na familia zilizowapa hifadhi  katika mitaa ya Goma.

UNICEF tayari inatoa misaada kwa mamia ya wanawake na watoto wanaotafuta hifadhi katika kituo cha Don Bosco Catholic Center huko Goma. Zicherman anasema UNICEF tayari ina mipango ya dharura  kwa sababu katika siku za nyuma ugonjwa wa kipindupindu  umewahi kuwa tatizo hapo huko Goma na  pia kwenye kambi ya Kanyaruchinya.

Category:

About GalleryBloggerTemplates.com:
GalleryBloggerTemplates.com is Free Blogger Templates Gallery. We provide Blogger templates for free. You can find about tutorials, blogger hacks, SEO optimization, tips and tricks here!

0 comments